Mradi wa majumba Kijani Ridge watunukiwa sifa
NA LAWRENCE ONGARO
TATU CITY imetangaza kukamilika kwa mradi wa ujenzi wa majumba ya Kijani Ridge uliogharimu takribani Sh1 bilioni.
Mkurugenzi mkuu wa Tatu City nchini Kenya, Bw Preston Mendenhall, alisema miradi ya aina hiyo iko pia katika nchi kadha za bara Afrika kama vile Zambia, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Rwanda na Ethiopia.
Alisema mradi huo hapa nchini umeshika kasi ambapo ni watu wengi watakaonufaika.
Alisema katika eneo la Tatu City kuna biashara zipatazo 70 kutoka kwa makampuni tofauti, shule za msingi na sekondari, viwanda vya kahawa miongoni mwa vingine.
“Tumekuwa katika biashara kuhusu miradi ya ujenzi kwa takribani miaka 15 na kwa hivyo Tatu City imeimarika sana,” alifafanua mkurugenzi huyo.
Kulingana na mpangilio uliopo katika mradi huo kuna barabara ya lami kilomita sita ndani ya eneo hilo la Kijani Ridge, huku kilomita 12 ikiwa ni sehemu ya wakazi kutembelea, huku kilomita tano kukiwa kuna mabomba ya maji yaliyopitishwa chini ya ardhi.
Halafu kuna kilomita 12 za nyaya za umeme zilizo kwenye ardhi huku kilomita 2.7 ikiwa ni bomba la majitaka.
Mradi huo umeendeshwa kwa muda wa miezi 14 mfululizo hasa katika eneo la Kijani Ridge.
Bw Mendenhall alisema mwanzoni mwa mwezi Macchi aliwaalika magavana 47 ambao baadhi yao walizuru Tatu City ili kupata mafunzo zaidi ya jinsi ya kupanua maendeleo katika kaunti zao.
“Nilifurahi kuwakaribisha magavana wapatao 30 ambao walipata mwelekeo mwafaka wa namna ya kupanua kaunti zao na kubuni ajira kwa vijana wengi wasio na kazi,” alifafanua mkurugenzi huyo.
Kijani Ridge inakalia sehemu ya ukubwa wa ekari 79 eneo la Crawford International, na Nova Pioneer School.
Alisema tayari asilimia 90 ya ujenzi wa majumba imekamilika ambapo yeyote anayetamani kununua ardhi katika eneo hilo ni kutoka ekari 1/4 na 1/2 ambapo ni kutoka Sh28 milioni.
“Eneo la Tatu City na vitongoji vyake kuna usalama wa kutosha ambapo yeyote anayetamani kupata sehemu ya kuishi ana haki ya kuishi kwa amani,” alieleza mkurugenzi huyo.