Spika Wetang’ula aharamisha kanuni ya CBK ya kudhibiti kiasi cha pesa cha kuwekwa benki na kutolewa
NA DAVID MWERE
SASA Wakenya watakuwa huru kuweka zaidi ya Sh1 milioni katika akaunti zao za benki, wakati mmoja bila kutoa maelezo kuhusu walikotoa pesa hizo.
Hii ni baada ya Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang’ula kuharamisha kanuni hiyo iliyowekwa na Gavana wa Benki Kuu ya Kenya (CBK) Patrick Njoroge.
Kwenye uamuzi wake ulioweka kwa tovuti ya bunge, Spika Wetang’ula alisema kanuni Dkt Njoroge aliamuru kanuni hiyo ianze kutekelezwa bila kuidhinishwa na Bunge kulingana na hitaji la Sheria Kuhusu Kanuni za Masharika ya Serikali.
“Kanuni yoyote inayotolewa chini ya mamlaka inayotolewa na Sheria ya Bunge sharti iletwe bungeni ili ikaguliwe,” Spika Wetang’ula akasema.
Kulingana na taarifa iliyotolewa na Gavana wa CBK Dkt Njoroge mwaka 2022, masharika ya kifedha kama benki hayafai kupokea zaidi ya Sh1 milioni kutoka kwa mteja bila mteja huyo kuelezea alikotoa pesa hizo.
Vile vile, mashirika hayo ya kifedha yamezuiwa kuruhusu wateja kutoa zaidi ya Sh1 milioni bila kutoa maelezo ya kuhusu matumizi ya pesa hizo.
Kama njia ya kufanikisha utekelezaji wa agizo hilo la CBK, watu wanaotaka kutoa kiwango kikubwa cha pesa wanahitajika kujaza fomu maalum itakayotolewa na Benki ili kuelezea mahala ambako pesa hizo zinapelekwa na mahala ambako zimetoka.
Ingawa lengo la CBK lilikuwa ni kudhibiti mwenendo wa kupitishwa kwa pesa haramu kama vile ulanguzi wa pesa na ufadhili wa ugaidi, miongoni mwa maovu mengine, kutoidhinishwa kwa kanuni hiyo na wabunge kunafanya utekelezaji wake kuwa haramu.
Kabla ya wabunge kwenda likizoni Desemba 6, 2022, Mbunge wa Ainabkoi Samuel Chepkonga aliomba ushauri kutoka kwa Spika Wetang’ula kuhusu mwenendo wa baadhi ya mashirika ya serikali kufeli kusaka idhini ya Bunge kabla ya kutekeleza kanuni mbalimbali.
Bw Chepkonga ni Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge kuhusu Sheria za Kanuni za Mashirika ya Serikali ambayo huchambua na kupendekeza kwa wabunge ikiwa wanapaswa kuidhinisha au kukataa kanuni zilizowasilishwa bungeni na mashirika ya kiserikali.
Bw Chepkonga haswa alimlenga Dkt Njoroge, akimshutumu kwa kufeli kuwasilisha kanuni za benki kuhusu viwango vikubwa vya kuweka na kutoa pesa na kwasilisha kanuni hizo bunge ili ziidhiishwe kabla ya kuanza kutekelezwa.
“Hofu ya kamati hii ni kwamba kuna kanuni nyingi ambazo zinatumika sasa lakini hazikuwasilishwa Bungeni inavyohitajika kwa mujibu wa Sheria kuhusu Kanuni za Mashirika ya Serikali ya 2013,” akasema Mbunge huyo wa Ainabkoi kwenye ombi lake kwa Spika Wetang’ula.
TAFSIRI: CHARLES WASONGA