Kaunti yasaidia wakazi kukata rufaa ya ardhi
Na Maureen Ongala
SERIKALI ya Kaunti ya Kilifi imeamua kutoa msaada wa kisheria kwa wakazi wa eneo la Kadzuhoni, Wadi ya Gongoni, katika eneo bunge la Magarini ili kutatua mzozo wa umiliki wa ardhi.
Gavana Amason Kingi aliwataka wakazi wa eneo hilo kushirikiana na Serikali ya Kaunti ili kupata mwafaka.Mzozo huo unahusisha umiliki wa ardhi ya ekari 300 ambayo inazozaniwa kati ya wenyeji na wawekezaji wanaodaiwa kumiliki kampuni ya kutengeneza chumvi eneo hilo.
Akizungumza katika mkutano na wakazi hao, Bw Kingi alisema Kaunti ilichukua jukumu la kukata rufaa, baada ya kuona kwamba wakazi hao hawakuwa wamepata haki katika uamuzi wa awali.
Uamuzi huo wa mahakama ulipelekea ubomoaji wa Shule ya Msingi ya Kadzuhoni na makazi ya baadhi ya wanakijiji.



