Serikali yaagizwa kujibu kesi kuhusu usiri wa SGR
NA PHILIP MUYANGA
MWANASHERIA Mkuu Kihara Kariuki, ameagizwa kujibu kesi ambapo wanaharakati wawili wanataka serikali iagizwe kutoa wazi habari kuhusu kiwango cha pesa kilicholipiwa deni ya ujenzi wa reli ya SGR.
Jaji John Mativo wa Mahakama Kuu ya Mombasa, amempa Mwanasheria Mkuu siku 14 kuwasilisha majibu yake.
Agizo sawa na hilo limetolewa kwa Shirika la Reli la Kenya na Mamlaka ya Ukusanyaji Ushuru Kenya.
Bw Caleb Ngwena na Bi Millicent Odhiambo, ambao ndio walalamishi, walitaka pia mawaziri wa fedha na uchukuzi waagizwe kutangaza kiasi cha pesa ambacho kimekusanywa kutoka kwa huduma za SGR tangu zilipoanzishwa hadi sasa.
Wawili hao walilalamika kuwa, mradi wa SGR ukiendelea kukumbwa na usiri bila uwajibikaji wa kifedha, haki zao za kikatiba pamoja na zile za wananchi wengine zinaendelea kukiukwa.



