Visa vya corona Mwamba RFC vyasababisha mechi yake na KCB kuahirishwa
Na GEOFFREY ANENE
MECHI ya Ligi Kuu ya raga ya wachezaji 15 kila upande (Kenya Cup) kati ya Mwamba na mabingwa watetezi KCB ugani Impala, imeahirishwa Jumamosi kwa sababu ya visa vya virusi vya corona.
Shirikisho la Raga Kenya (KRU) limesema mchuano huo umeondolewa “kwa sababu ya masharti ya kiafya na usalama”.
Hata hivyo, imebainika kuwa sababu ya mechi hiyo kuahirishwa ni kuwa Mwamba maarufu kama Kulabu, imeshuhudia visa vingi vya maambukizi ya corona.
“Sisi tayari tulikuwa tumefika uwanjani kuvaana na Mwamba tulipofahamishwa kuwa mechi imeahirishwa. Mwamba ina visa vingi vya corona. Ilikuwa mechi yetu ya mwisho 2021 kabla ya kuenda likizo ya Krismasi,” Mwenyekiti wa KCB RFC Xavier Makuba alieleza Taifa Leo Jumamosi adhuhuri.
Michuano mingine iliyopangiwa kusakatwa Desemba 18 ni Kenya Harlequin kualika Homeboyz ugani RFUEA, Nondescripts kupimwa vilivyo na Strathmore Leos (Ngong Racecourse), Blak Blad ya Chuo Kikuu cha Kenyatta kupepetana na wenyeji To Fry Nakuru (Nakuru Athletic) na Chuo Kikuu cha Masinde Muliro (MMUST) kuonyeshana ubabe dhidi ya Menengai Oilers mjini Kakamega. Tukienda mitamboni, mechi pekee iliyoahirishwa ni kati ya Mwamba na KCB.
Next article


