– Mutahi alisema eneo la Mlima Kenya linamuogopa DP Ruto na hivyo walitafuta mbinu ya kummaliza
– Alisema eneo hilo lilimshabikia kisiasa ili aweze kujichimbia kaburi lake la kisiasa kabla ya 2022
– DP Ruto amekuwa akionekana kusongwa na masaibu ya kisiasa huku ripoti zikiarifu kuna tofauti za kisiasa kati yake na Rais Kenyatta
Mchanganuzi wa kisiasa Mutahi Ngunyi amesema eneo la Mlima Kenya lilifanya njama ya kumshabikia Naibu Rais William Ruto ili aanze kujiangamiza kisiasa.
Alisema hiyo ndiyo sababu Ruto amekuwa akionyeshwa uungwaji mkono katika eneo hilo tangu waungane na Rais Uhuru Kenyatta.
Naibu Rais William Ruto. Mutahi Ngunyi alisema Mt Kenya iliamua kumshabikia DP Ruto ili ajiangamize kisiasa. Picha: Citizen Source: Facebook
Kupitia mtandao wake wa twitter Jumatatu, Julai 13, Mutahi alilinganisha ufuasi wa DP katika eneo hilo na kuchimba shimo la kisiasa.
Aidha, alisema eneo hilo limekuwa likimuogopa DP na ndipo likaweka mikakati ya jinsi watamuangusha.
“Huku wakimhofia Ruto, mikakati ya GEMA ilikuwa kumshabikia na kisha kumuangusha. Mara tu ambapo huanzia jambo kutoka juu ni wakati ambapo unachimba shimo,” alisema Ngunyi.
Ngunyi aliyasema hayo wakati ambapo DP anaonekana kukumbwa na mawimbi ya kisiasa haswa baada ya ripoti za mwanya wa kisiasa kati yake na Rais Uhuru Kenyatta.
Wandani wa DP wamekuwa wakitimuliwa kwenye nyadhifa zao katika chama cha Jubilee katika vita vinavyoongozwa na Rais Uhuru Kenyatta.