– Nzoia Sugar FC, kilizawadiwa basi jipya lenye uwezo wa kuwabeba watu 52, na Rais Uhuru Kenyatta siku ya Jumatano, Julai 1
– Rais alimkabithi Mwenyekiti wa Kampuni ya Sukari ya Nzoia basi hilo ambalo litakuwa likitumiwa na klabu hiyo kwa shughuli zao za soka
– Hafla hiyo iliandaliwa katika Jumba la Harambee jijini Nairobi ambapo Uhuru alikutana na viongozi kutoka eneo la Magharibi mwa Kenya kujadili miradi ya maendeleo
Klabu cha Ligi Kuu ya Kenya, Nzoia Sugar FC, kilizawadiwa basi jipya lenye uwezo wa kuwabeba watu 52, na Rais Uhuru Kenyatta siku ya Jumatano, Julai 1.
Rais alimkabithi Mwenyekiti wa Kampuni ya Sukari ya Nzoia, Joash Wamang’oli basi hilo ambalo litakuwa likitumiwa na klabu hiyo kwa shughuli zao za soka.

Rais Uhuru alizawadi Nzoia FC basi jipya lenye uwezo wa kuwabeba watu 52. Picha: Nzoia FC.
Source: Twitter
Kikosi hicho pia kilitunukiwa KSh2 milioni kutoka wa Rais katika hafla ambayo iliandaliwa katika Jumba la Harambee jijini Nairobi ambapo Uhuru alikutana na viongozi kutoka eneo la Magharibi mwa Kenya kujadili miradi ya maendeleo.
Viongozi ambao walihudhuria hafla hiyo ni ikiwemo magavana Wycliffe Oparanya (Kakamega), Sospeter Ojaamong (Busia), Wycliffe Wangamati (Bungoma), Wilbur Ottichilo (Vihiga) na Patrick Khaemba (Trans-Nzoia).
Viongozi wengine kutoka eneo la magharibi ambao walihudhuria hafla hiyo ni pamoja na Waziri wa Ugatuzi, Eugene Wamalwa na Katibu Mkuu wa COTU, Francis Atwoli.
Mwenyekiti wa klabu hiyo Evans Kadenge, ambaye ni mwanawe marehemu Joe Kadenge, alimshukuru Kiongozi wa Taifa na kuahidi kuwa timu hiyo itaandikisha matokeo bora katika msimu mpya wa KPL ambao unatazamiwa kung’oa nanga mwezi Agosti.
Klabu hicho kilikuwa kimezoa pointi 13 baada ya kushiriki mechi 22 kabla ya kuzuka kwa janga la virusi vya corona ambalo lilitatiza shughuliza michezo duniani.