Wakazi wa eneo la Lugulu, kaunti ya Bungoma walijionea sinema ya bwerere baada ya mrembo kumfukuza jamaa aliyemfuata kwao licha yao kutengana.
Semasema za mtaani ziliarifu kuwa wawili hao walikuwa wameona kwa muda lakini kutokana na mizozo ya mara kwa mara katika ndoa mrembo aliamua kurejea nyumbani kwa wazazi wake.
Hata hivyo, inasemekana wazazi walimrai mwanao ampe jamaa makaribisho mazuri na kisha ampe kiti ndiposa aweze kujieleza vizuri.
Hata hivyo kidosho aliyekuwa na hamaki alisimama na kuanza kumkaripia jamaa akiwaarifu wazazi wake jinsi alivyoteseka mikononi mwake.
“Kukaribisha nani? Huyu hana akili hata kidogo. Amenitesa sana huyu kwa muda mrefu. Hata chupi pekee hajawahi ninunulia lakini hawara wake ndio wanazidi kunenepa. Wacha asimame hapo aseme kile anataka,” demu alifoka.
Maneno ya demu yalimduwaza jamaa lakini hata hivyo, alijaribu kila awezalo kumshawishi kipusa arejee kwake ili waweze kusuluhisha mizozo iliyokuwepo baina yao.
“Mimi sina vimada. Rudi nyumbani sababu naumizwa na baridi,” lofa alimsihi demu.
“Wewe ni kama unasumbuliwa na bangi. Toa hicho kitambi chako hapa haraka. Sitaki kukuona hapa tena na kamwe sirudi kwako,” dada alisema.
Baadaye aliingia chumbani ambapo alichomoka na mpini wa jembe na kumtimua polo ambaye hakuwa na lingine ila kukimbilia usalama wake.
Kisanga hicho kiliwavunja mbavu majirani ambao walikuwa wamekusanyika kujionea yaliyojiri.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia [email protected] au WhatsaApp: 0732482690.