-Ubomoaji huo ulitekelezwa chini ya ulinzi mkali wa polisi ili kupenyeza mwanya wa ujenzi wa barabara
-Katika picha, waathiriwa walionekana wakitazama kwa huzuni shughuli hiyo bila kutambua cha kufanya
-Haya yanakujia wiki mbili baada ya moto mkubwa kuteketeza sehemu ya soko hilo
Baadhi ya wafanyabiashara wa Soko la Gikomba, jijini Nairobi, waliamka Jumanne, Julai 14 asubuhi, na kupata vibanda vyao vimebomolewa, wiki mbili baada ya moto mkubwa kuteketeza sehemu ya soko hilo.
Ubomoaji huo ulitekelezwa chini ya ulinzi mkali wa polisi ili kupenyeza mwanya wa ujenzi wa barabara katika eneo hilo.
Moto huo uliteketeza sehemu ya soko hilo huku vibanda vya nafaka na vya kuweka nguo za mitumba vikiathirika pakubwa.
Chanzo cha moto huo hakukubainika lakini Wakenya ambao wamekuwa wakishuhudia tukio hilo kila mara wameelekeza kidole cha lawama kwa wanyakuzi wa ardhi jijini.
Serikali kupitia kwa Katibu Mkuu wa Usalama wa Ndani, Karanja Kibicho iliahidi kuwafidia waliopoteza mali yao katika moto huo na kutangaza kuwa uchunguzi unaendelea.
Kibicho pia aliwaonya wahuni wanaohangaisha wafanyabiashara wa soko la Gikomba kupitia mikasa ya moto inayoshuhudiwa mara kwa mara.
Katibu huyo alibainisha kuwa kuwa ardhi ya Gikomba ni mali ya umma na kwamba haihusishwi kwa vyovyote vile na wawekezaji binafsi.
Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia [email protected] au WhatsaApp: 0732482690.