-Hall ni kocha wa tano kugura klabu hiyo msimu huu baada ya wengine wanne waliomtangulia
– Muingereza huyo aliondoka Wazito FC kwa kuafikiana na uongozi wa klabu hiyo
– Stewart alisema kuwa anajivunia kuondoka klabu hiyo huku akiwa ameimarisha kikosi cha Wazito FC
Kocha Muingereza, Stewart Hall amegura klabu ya Ligi Kuu ya Kenya, Wazito FC kupitia maafikiano.
Mkufunzi huyo mwenye tajriba alitangaza kujiuzulu kwake siku ya Jumatatu, Julai 6, katika taarifa kupitia tuvuti rasmi ya klabu hicho.

Kocha Stewart Hall alisema anajivunia ufanisi aliyopata katika kipindi Wazito FC. Picha: The Standard.
Source: UGC
Stewart alisema kuwa anajivunia kuondoka klabu hiyo huku akiwa amefanikiwa kutimiza mengi katika kipindi chake klabuni humo.
“Ningependa kuthibitisha kuwa tumefikia makubaliano na Wazito FC kuhusu kuondoka kwangu klabuni.Wakati nilijiunga na klabu hii Novemba, majukumu yangu yalikuwa kuimarisha timu na kuwasajili wachezaji ambao wangepiga klabu jeki,”
“Pamoja na kikosi changu cha ushauri, tulifanya kazi kwa bidii, wachezaji walitimiza wajibu wao na pamoja tuliandikisha matokeo bora,” alisema Hall.
Hall pia alishukuru uongozi wa klabu hiyo, wachezaji na kikosi cha ushauri kwa kuhakikisha kuwa anapata mazingira bora.
Kocha huyo wa zamani wa AFC Leopards na Sofapaka, pia alidokezea kuwa atarejea nchini Uingereza hii karibuni kujumuika pamoja na familia yake.

Hall alisifiwa kwa kuimarisha kikosi cha Wazito FC. Picha: UGC.
Source: Twitter
Afisa Mkuu Mtendaji wa Wazito FC, Dennis Gicheru alithibitisha kuondoka kwa Muingreza huyo huku akimlimbikizia sifa sufufu kwa kazi bora aliyofanya klabuni humo.
“Ningependa kumshukuru Stewart kwa mchango wake klabuni. Aliwasili wakati ambapo tulikuwa tunahangaika sana na hatua kwa hatua alibuni timu imara na nina uhakika kuwa mrithi wake atapata timu bora. Tunamtakia kila la heri siku zake za usoni,” alisema Gicheru
Gicheru pia alidokezea kuwa klabu hiyo itatangaza kikosi kipya cha ushauri hii karibuni.
Hall ni kocha wa tano kugura klabu hiyo msimu huu baada ya Stanley Okumbi, Fred Ouna, Hamisi Abdalla na Melis Medo kuondoka.
Klabu hiyo kwa sasa inashikilia nafasi ya 13 kwenye msimamo wa KPL na pointi 20 kutoka kwa mechi 23 walizoshiriki.